BLOG HII IMEDHAMINIWA NA: MWEKASU HOSTEL, PWEZA NIGHT CLUB TANGA, SOPHIA PRODUCTION, AFRICAN DESIGN, BREEZE FM, PANGANI COAST CULTURAL TOURISIM PROGRAMME, NA SAFARI LODGE ANNEX
Photobucket

Friday, September 24, 2010

'NITARUDISHA HESHIMA YA MKOA WA TANGA'- ASEMA LIPUMBA!

MGOMBEA urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chama cha Wananchi CUF Profesa Ibrahim Lipumba amefufua matumiani ya wananchi wa Tanga na kuweka bayana kuwa atakapochaguliwa atahakikisha sekta ya viwanda mkoani Tanga inaimarika.

Akihutubia maelfu ya wakazi wa Tanga katika uwanja wa Tangamano,Profesa Lipumba ameahidi kurejesha heshima ya Mkoa wa Tanga iliyoporomoka kwa viwanda vingi kufa huku ikishuka kwenye chati za mikoa maarufu kiuchumi kutoka nafasi ya pili hadi 16.

Amewaeleza wakazi wa Tanga kuwa atakapoingia madarakani atahakikisha hadhi ya Tanga inarudi kwa kuvifufua viwanda vilivyokufa na kueleza kuwa hayo yatawezekana ikiwa atachaguliwa kuingia ikulu.

Pia amezungumzia juu ya uboreshaji wa elimu hasa masomo ya sayansi kwa kuwawezesha kupatikana walimu watakaokuwa na uwezo wa kufundisha masomo hayo ili kuongeza idadi ya wanasayansi kwani ulimwengu huu ni wa sayansi.

Amewataka wananchi wa Tanga kuchagua madiwani wa chama hicho ili kuunda baraza la madiwani litakalosimamia fedha za miradi ya maendeleo ili wananchi waweze kunufaika na fedha hizo.

Awali Mgombea Ubunge wa CUF,Bw.Mussa Mbaruku amewataka wananchi kumpa kura ili kupata mtetezi wa kweli katika bunge kwani jimbo la Tanga kwa muda mrefu sasa limekosa uwakilishi wa kweli bungeni.


No comments:

Post a Comment